" Kuanza kwa huduma katika zahanati hii ya Mihama ni ukombozi katika sekta ya afya kwetu sisi wana Mihama lakini hata kwa wageni na wakazi wa maeneo ya jirani ambao tumekuwa tukihangaika kwa muda mrefu kupata huduma za afya hospitali ya Sekoutoure,uwepo wake unaakisi takwa la ilani ya Chama Cha Mapinduzi na ahadi tuliyoitoa kwa wananchi mwaka 2020/2025.Tunajivunia kutimiza ahadi yetu kwa wakati kabisa."
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa CCM kata ya Kitangiri Enos Hange Masalu wakati akipokea wageni kutoka TASAF makao makuu Dodoma wanaoendelea na ziara yao ya siku tatu kukagua na kutembelea miradi mbalimbali inayoendelea kutekelezwa ndani ya Manispaa ya Ilemela kupitia mradi wa kupunguza kaya maskini TASAF.
Akizungumzia suala la ushiriki wa jamii katika mradi huo Mwenyekiti wa kamati ya usimamizi wa mradi mtaa wa Mihama Elias Nyanda amesema jamii imeshiriki kikamilifu kwani ilipangiwa kuchangia kiasi cha shilingi milioni 10.3 na mpaka sasa imechangia kiasi cha shilingi milioni 10.2.
" Naushukuru uongozi wote wa Wilaya kuanzia Mbunge wetu Mhe.Angeline Mabula,Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Mhe.Hassan Elias Masala, wataalam kutoka Manispaa na baraza la madiwani kwa kuendelea kunipigania kata ya Kitangiri kupata miradi zaidi ya maendeleo,mradi huu utakuwa msaada mkubwa kwa wananchi wote."
Nae mratibu wa mradi wa TASAF Ilemela Leonard Nyamgenda Robert amefafanua kuwa mradi umegharimu jumla ya kiasi cha shilingi milioni 187 ambapo mpaka sasa umefikia asilimia 98 ya utekelezaji wake.
Aidha mradi wa ujenzi wa barabara ya Kabuhoro ndani ya kata ya Kirumba yenye urefu wa mitaa 780 ulitembelewa pia huku kukamilika kwake kukitajwa kurahisisha usafiri katika eneo hilo.
Akihitimisha ziara hiyo Mkuu wa kitengo cha habari na mawasiliano TASAF Bi.Zuhura Mchungi amepongeza kazi inayoendelea.
" Hongereni kwa kazi nzuri jukumu letu ni moja tu kuhamasishana katika kuilinda na kuitunza miundo mbinu hii,tukumbuke hii ni fedha imewekwa hapa ni lazima tuonyeshe umiliki wa miradi yetu.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela
Postal Address: 735 MWANZA
Telephone: + 255 736 200910
Mobile:
Email: md@ilemelamc.go.tz
Copyright ©2017 Ilemela Municipal Council . All rights reserved.