Ikiwa ni siku ya maadhimisho ya mtoto wa Afrika ambayo huadhimishwa kila mwaka siku ya tarehe 16 mwezi juni, watoto wa wilaya ya Ilemela wameungana na mataifa mengine barani Afrika kuadhimisha siku ikiwa ni kumbukizi ya maandamano ya watoto wa soweto, Afrika Kusini mwaka 1976 ambapo walipinga suala la ubaguzi wakipambania haki zao za msingi.
Lengo kuu la maadhimisho haya ni kuongeza uelewa kuhusu hali ya watoto wa afrika na kuhimiza utekelezaji wa haki zao kama ilivyoainishwa katika ibara ya 2 hadi ya 22 ya mkataba wa Afrika wa haki na ustawi wa mtoto.
Chini ya Kauli mbiu ya mwaka huu 2025 inayosema “Haki za Mtoto; Tulipotoka, Tulipo na Tuendako”, inawataka wazazi, walezi, serikali na wadau wengine mbalimbali kutathmini mafanikio yaliyopatikana na changamoto zinazokwamisha utekelezaji wa haki za mtoto,kwa kuzingatia wajibu wao katika kuimarisha mifumo ya ulinzi na maendeleo ya Mtoto.
Akimwakilisha aliyekuwa mgeni rasmi ambae ni Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Mhe Hassan Masala, Bi Anna Mbao Afisa Tawala wa wilaya ya Ilemela amewapongeza watoto hao kwa kuadhimisha siku yao hii muhimu na kusisitiza kuwa jukumu la ulinzi wa mtoto linaanza na mtoto mwenyewe hivyo kuwataka wasisite kuzipigania haki zao kwa kutoa taarifa kwa wakati pale haki zao zinapokiukwa na kuhakikisha wanajilinda na kutambua misingi wanayotakiwa kuishi.
"Serikali inatambua umuhimu wa watoto ndio maana imeweka miongozo na sheria mbalimbali ,kwa ajili ya kuwalinda na kuwatetea watoto ili tuweze kupata watoto wenye akili wanaojitambua watakayoyaishi wanayoelekezwa ili tutengeneze taifa bora la baadae, hivyo mkaishi elimu mliyopatiwa", amesisitiza Bi Anna
Nae mkurugenzi wa halmashauri ya manispaa ya Ilemela Bi Ummy Wayayu amewaasa na kuwataka watoto kuwa walinzi wa kwanza wa unyanyasaji wanaofanyiwa kabla ya watu wengine kuwa walinzi kwao kwa sababu wao ndio waathirika wa kwanza wa unyanyasaji
Kupitia Risala ya watoto iliyosomwa na mtoto Aziza Malilo kwa niaba ya watoto wenzake wameiomba serikali kuendelea kupambana na kuongeza nguvu zaidi katika kutekeleza haki za watoto, kupatiwa elimu pasipo kubaguliwa sambamba na kuendelea kuwekeza katika watoto
Maadhimisho ya siku ya mtoto wa Afrika katika wilaya ya Ilemela kwa mwaka 2025 yalipambwa na matukio mbalimbali kama vile bunge la watoto ambapo walipata fursa ya kuzielezea changamoto zao, sambamba na kwaya, maonyesho , na shairi.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela
Postal Address: 735 MWANZA
Telephone: + 255 736 200910
Mobile:
Email: md@ilemelamc.go.tz
Copyright ©2017 Ilemela Municipal Council . All rights reserved.