Kuelekea maadhimisho ya siku ya mazingira duniani ambayo huadhimishwa Tarehe 05 Juni kila mwaka, rai imetolewa kwa wananchi wa Ilemela kufanya usafi kuwa ni tabia ya kila siku na sio kusubiria maagizo ya serikali.
Rai hiyo imetolewa na Bi Anna Mbao akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Mhe Hassan Masala wakati wa kampeni ya usafi kila Jumamosi ya Mwisho wa mwezi iliyofanyika Soko la kiloleli kata ya Ibungilo mapema hii leo tarehe 31 Mei 2025
"Usafi ni tabia, tufanye usafi kuwa ni tabia ya kila siku na sio hadi tusubiri maelekezo ya serikali, kila mtu ajijengee tabia ya kufanya usafi"amesema Bi Anna
Bi Anna akiongea na wananchi wa Ilemela kupitia wafanyabiashara wa soko la Kiloleli ameendelea kuwasisitiza juu kudhibiti matumizi ya bidhaa za plastiki kwa ajili utunzaji wa mazingira na viumbe hai wanaoishi kwenye vyanzo vya maji huku akiwashukuru kwa kujitokeza kwao katika zoezi hili la usafi.
Nae Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela Bi. Ummy Wayayu amesisitiza juu ya utunzaji wa mazingira katika jamii hususan katika maeneo ya biashara za chakula ili kuepukana na magonjwa ya mlipuko yanayotokana na uchafuzi wa mazingira.
“Sambamba na zoezi hili la usafi wa leo niendelee kuwaahidi kuwa tutaendelea kuboresha miundombinu ya soko hili kama tulivyoanza kuboresha eneo la kuuzia ndizi ili muendelee kufanya biashara kwa amani huku tukiinua uchumi wa nchi yetu” Alisema Bi Ummy
Kwa niaba ya wafanyabiashara wa soko la Kiloleli, Ndugu Hakim Katabazi ambae ni Makamu mwenyekiti wa soko wamemshukuru Mkurugenzi wa Ilemela kwa kuanza kutekeleza ahadi ya ujenzi wa eneo maalum la kuuzia ndizi huku wakiomba uboreshaji zaidi wa soko ili liwe na hadhi ya kitaifa sambamba na kuushukuru uongozi wa wilaya Ilemela kwa kujumuika na wafanyabiashara wa soko hilo katika zoezi la usafi wa mwisho wa mwezi, na kusema kuwa usafi ni jadi yao.
Kauli mbiu ya siku ya mazingira dunianni ambayo kitaifa itaadhimishwa mkoani Dodoma siku ya tarehe 5 Juni, inasema;"Mazingira yetu na Tanzania ijayo,tuwajibike saa;Dhibiti matumizi ya Plastiki.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela
Postal Address: 735 MWANZA
Telephone: + 255 736 200910
Mobile:
Email: md@ilemelamc.go.tz
Copyright ©2017 Ilemela Municipal Council . All rights reserved.