“Serikali itaendelea kujiimarisha katika kuboresha upatikanaji wa huduma bora kwa wazee kwa kuzingatia umuhimu wa kundi hili katika jamii yetu ya Tanzania”
Hayo yamesemwa na mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Bi.Neema Kipeja katika maadhimisho ya siku ya wazee duniani ambayo huadhimishwa tarehe moja mwezi wa kumi ya kila mwaka.
Aidha alisema kuwa Serikali inatambua kuwa wazee ni hazina katika kuibua na kuchochea shughuli mbalimbali za kimaendeleo kutokana na ushauri mzuri wanaotoa wanaposhirikishwa katika mambo ya kimaendeleo.
Aliendelea kusema kuwa Serikali ya awamu ya sita inaendelea kuthibitisha kuwajali wazee kwa kuboresha mradi wa kusaidia kaya maskini (TASAF) ambapo wazee wote wenye vigezo wameombwa kujitokeza kwenye ofisi za jirani za serikali ili kutambuliwa na kuingizwa kwenye mpango huo.
Pamoja na hayo, Bi. Neema amewahimiza wazee kuwa na utaratibu wa kwenda kucheki afya zenu mara kwa mara ili kupata huduma stahiki kwa wakati kwani huduma za afya kwa wazee kuanzia miaka 60 ni bure katika vituo vyote vya kutolea huduma.
Kupitia maadhimisho hayo Bi. Neema alitumia fursa hiyo kuwakumbusha wazee hao juu ya UVIKO-19 na kuwataka wazee kuendelea kuchanja, kwani wapo kwenye kundi ambalo ni rahisi kupata maambukizi hayo huku akiwatoa hofu kwamba chanjo hii ni salama kabisa na kuwataka kumuunga mkono Mhe.Rais alieona umuhimu wa kuokoa maisha ya watanzania kwa kupata chanjo hii.
Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo kiwilaya ndani ya kata ya Bugogwa, Mzee Jackson Kabote ambaye ni katibu wa baraza la wazee wilaya ya Ilemela amezitaja baadhi ya changamoto zinazowakabili wazee ikiwa ni pamoja upungufu wa dawa na wa wataalam wa kuhudumia wazee,umaskini uliokithiri kutokana na kipato duni au kutokuwa na kipato kabisa sambamba na wazee kutokupewa kipaumbele kama makundi mengine kama vile wanawake,vijana na walemavu.
Halmashauri ya manispaa ya Ilemela imeungana na Halmashauri nyingine nchini Tanzania kuadhimisha siku ya wazee duniani ikiwa ni kumbukizi ya kila mwaka ya siku ya wazee duniani iliyorasimishwa na shirika la kimataifa (UN)miaka 35 iliyopita,ikiambatana na kauli mbiu ya. “matumizi sahihi ya kidigitali kwa ustawi wa rika zote”.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela
Postal Address: 735 MWANZA
Telephone: + 255 736 200910
Mobile:
Email: md@ilemelamc.go.tz
Copyright ©2017 Ilemela Municipal Council . All rights reserved.