Wito umetolewa na Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilemela, Mhandisi Modest Apolinary kwa wajumbe wa mabaraza ya usuluhishi ya kata kuhakikisha wanatenda haki kwa wananchi ili kuweza kupunguza malalamiko yanayotoka kwa wananchi.
Mhandisi Modest ametoa wito huo wakati wa zoezi la kuwaapisha na kutoa mafunzo kwa wajumbe hao wa mabaraza ya usuluhishi ya kata
“Niwaombe mkatende haki, msiende kutumia fedha za wale wenye nazo kuchukua ardhi ya wale wasio na fedha ili wote kwa pamoja tupunguze malalamikio ya wananchi,nyie mnajua haki kwasababu ni wenyeji wa maeneo hayo mnajua historia ya maeneo yenu mnajua mwenye haki ni nani kwanini mwenye haki ananyimwa haki anapewa asie na haki”, Amesisitiza Mkurugenzi.
Pamoja na wito huo, Mhandisi Modest ameweka bayana kuwa iwapo itabainika kuwa iwapo miongoni mwa mabaraza haya itabainika hayatendi haki na kujiridhisha basi hatosita kuyavunja na kutafuta viongozi wengine wataoendana na taratibu huku akitoa mfano kwa baraza la kata la Kirumba ambalo lilivunjwa baada ya kubainika kwa vitendo vya rushwa.
Aidha amewataka wajumbe hao kuanza kazi mara moja baada ya kuapishwa kwani wananchi wanasubiria kusuluhishwa migogoro yao. Sambamba na hilo amesemea kuwa Ilemela zipo changamoto kubwa za migogoro ya ardhi ambayo iko kwao hivyo angependa kuona wananchi wanapokuja kulalamika kwake wanakuja na maoni ya mabaraza ja,mbo ambao pia litamsaidia Mwenyekiti wa baraza la ardhi la wilaya kutoa hukumu iliyo sahihi.
Wakili Patrick Muhere ambae ni Mwanasheria wa Manispaa, kabla ya kuwaapisha wajumbe hao amewaelekeza kuwa kazi yao kubwa ni kusuluhisha na sio kutoa maamuzi na kufafanua zaidi kuwa mabaraza kazi yake ni kusikiliza malalamiko ya wadaawa (ambao ni mlalamikaji na mlalamikiwa) wanasemaje, na kusisitiza kuwa hawaendi kufanya maamuzi kwani kwa kufanya hivyo watawaingiza kwenye gharama kwani wakikata rufaa kwa Mwenyekiti hukumu itafutwa na ataangalia kama hatua zilifuatwa
“Kazi yenu kubwa ni kusuluhisha na sio kutoa maamuzi, baraza kazi yake ni kusikiliza malalamiko ya wadaawa ambao ni mlalamikaji na mlalamikiwa wanasemaje hivyo hatufanyi kwa utashi bali tunafanya kwa mujibu wa sheria”, amefafanua wakili Muhere
Ndugu Mayeye Magambo Mwenyekiti wa baraza la ardhi la nyumba mkoa wa Mwanza ametoa angalizo kwa wajumbe hao kuwa sheria ya mabaraza ya kata imetoa siku 30 kuwa wamefanya usuluhishi na iwapo pande mbili zitakuwa hazijaridhika hawatatakiwa kukata rufaa bali wapewe hati ya kukosa usuluhishi na wafike baraza la wilaya ambapo watawasikilizwa kwa kuita mashahaidi baada ya kufungua maombi.
Ndugu Mayeye amewahimiza kuwa kazi yao ni kusikiliza pande zote mbili kwa kutumia busara na hekima na wahakikishe wanatumia vipawa walivyojaaliwa na Mwenyezi Mungu katika kuwapatanisha watu wenye migogoro na kumaliza migogoro kwa amani na upendo ili amani iendelee kudumu katika kata na watu waendelee kuishi bila migogoro.
Asia Mkandala na ndugu Mchunguzi ni wajumbe kutoka mabaraza ya kata za Nyamanoro na Pasiansi wao wameshukuru kwa kuapishwa kwao na kupewa mafunzo mafupi na kuahidi kuwa watatenda kazi kutokana na miongozo bila kukiuka maelekezo waliyopatiwa kwa kushirikiana na wajumbe wenzao kutekeleza majukumu yao ya usuluhishi kwa kutenda haki bila ya upendeleo wowote na bila kuvuka mipaka ya miongozo kwa hekima na busara huku wakiishukuru serikali kwa kuwapunguzia majukumu ya mabaraza.
Wajumbe 141 wa mabaraza ya usuluhishi ya kata wameapishwa ambapo jukumu kubwa la mabaraza haya ni kusuluhisha migogoro ndani ya kata zao inayohusiana na ardhi, ndoa na kushughulikia makossa ya jinai yatokanayo na ukiukwaji wa sheria ndogo za Halmashauri.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela
Postal Address: 735 MWANZA
Telephone: + 255 736 200910
Mobile:
Email: md@ilemelamc.go.tz
Copyright ©2017 Ilemela Municipal Council . All rights reserved.