Mbunge wa Jimbo la Ilemela na Naibu Waziri wa ardhi,Nyumba ,Maendeleo ya Makazi, Mhe.Daktari Angeline Mabula amewahimiza wananchi kuwa wazalendo na kuhakikisha kuwa wanalipa kodi kwa ajili ya kujjiletea maendeleo.
Ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na wananchi wa mitaa ya Gedeli na Nyakato sokoni iliyopo katika kata ya Nyakato katika ziara ya kikazi jimboni. Ametumia fursa ya ziara hiyo kuwasisitiza juu ya umuhimu wa kulipa kodi ili Serikali iweze kuwahudumia na kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo
“ Ili kuweza kupata huduma za kijamii pamoja na kuwa na maendeleo mbalimbali sisi wananchi tunatakiwa kuwa wazalendo kwa kuhakikisha kuwa tunalipa kodi kwani huo ni wajibu wetu sote”, alisisitiza
Aidha, ameipongeza idara ya Ardhi ya Manispaa ya Ilemela kwa juhudi kubwa wanazoendelea nazo katika kushughulikia kero na migogoro mbalimbali ya ardhi huku akiwahakikishia wananchi wake kuwa hakuna ucheleweshwaji wa hati miliki kama utakuwa umekidhi vigezo na masharti yote muhimu yanayohitajika.
Kwa upande wake afisa ardhi wa Manispaa ya Ilemela, Shukrani Kyando amewataka wananchi waliokwisha milikishwa viwanja kuhakikisha wanavilinda na kusisitiza kuwa si jukumu la serikali kisheria kulinda kiwanja cha mtu baada ya kumilikishwa.
Nae Diwani wa kata ya Nyakato Mhe. Alfred Wambura amemshukuru mbunge huyo kwa kuipa nafasi ya kipekee kata yake kwa kukubali kufanya mikutano miwili kwa siku moja katika mitaa miwili tofauti ya kata ya Nyakato huku akiahidi kumuunga mkono kwa kumpa ushirikiano.
Ziara hii ya Mbunge wa Ilemela, ni muendelezo wa ziara zake ikiwa ni utaratibu aliojiwekea wa kutembelea kata zilizopo katika jimbo lake kwa ajili ya kukagua miradi ya maendeleo, kusikiliza na kutatua kero mbalimbali za wananchi pamoja na kuongea na wananchi wa kata hizo.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela
Postal Address: 735 MWANZA
Telephone: + 255 736 200910
Mobile:
Email: md@ilemelamc.go.tz
Copyright ©2017 Ilemela Municipal Council . All rights reserved.