Na Paschalia George, Afisa Habari
Takribani viwanja 2000 vitapimwa katika mitaa ya Nyamiswi, Igalagala, Sangabuye, Nyafula na Ilekako Isanzu na Igogwe katika kata za Sangabuye na Bugogwa za Halmashauri ya Ilemela.
Upimaji wa viwanja hivi ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa kupima, kupanga na kumilikisha ardhi katika Manispaa ya Ilemela kupitia fedha za mkopo usio na riba kiasi cha shilingi Bil.3.6 kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Katika hatua za awali za utekelezaji wa mradi mikutano na wananchi wa mitaa husika imefanyika yenye lengo la kutambulisha, kuelimisha na kuhamasisha jamii juu ya ujio wa mradi huo.
Akizungumza katika moja ya mikutano hiyo, Francis Mwangwa, Afisa Mipangomijji wa Manispaa ya Ilemela alieleza kuwa, nia ya serikali ni kuhakikisha miji yote nchini inapangwa vizuri kwa kuzingatia sheria za mipango miji sambamba na kuhakikisha huduma zote za msingi za kijamii kama vile uwepo wa maeneo ya makaburi,shule,hospitali na masoko vinapatikana.
“Zoezi hili ni la lazima kwetu kwa sasa kutokana na ongezeko la watu na ukuaji wa haraka wa manispaa yetu”,Alisema Mwanga akiongeza kuwa wananchi wote wenye maeneo katika eneo la mradi watapewa kipaumbele kubaki katika maeneo yao kwa utaratibu maalum sambamba na kulipwa fidia stahiki ili kupisha shughuli za maendeleo kwa faida ya wengi.
Aidha ilielezwa kuwa ipo miongozo na sheria za ardhi itakayofatwa katika zoezi zima la kuthaminisha ardhi na mali zake na kuwa hakuna mwananchi atakaedhulumiwa au kuonewa hivyo wananchi wametakiwa kuwa na uvumilivu katika kipindi cha zoezi hili hususan uthamini ambao unatarajiwa kuanza hivi punde.
Juma Shija ni mkazi wa mtaa wa Isanzu ameshukuru kwa ujio wa mradi huo huku akisistiza ulipwaji wa fidia uwe kwa wakati ili kuruhusu watu kuanzisha shughuli zingine za kiuchumi kwani wananchi wengi wa maeneo hayo wanaishi kwa kutegemea ardhi zao kwa shughuli za kilimo.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela
Postal Address: 735 MWANZA
Telephone: + 255 736 200910
Mobile:
Email: md@ilemelamc.go.tz
Copyright ©2017 Ilemela Municipal Council . All rights reserved.